Ijumaa 11 Septemba 2026 - 18:05
Bila kukomesha vyombo vya ukandamizaji, mageuzi ya kweli yatabakia kuwa ni kauli tupu

Hawzah/ Kituo cha Haki za Binadamu Bahrain kimezitaka mamlaka kuchukua hatua za haraka za kuacha “kuwateka na kuwatesa watu” na kuwafikisha mbele ya sheria wale wanaohusika na uhalifu wa mateso.

Kwa mujibu wa Idara ya tarjama ya Shirika la Habari la Hawza, Kituo cha Haki za Binadamu Bahrain kimezitaka mamlaka za Bahrain kusitisha mara moja vitendo vya kuwateka na kuwatesa watu, kuweka wazi hatima na mahali walipo watu wote waliopotezwa kwa lazima, na kuhakikisha kesi za kweli na zenye ufanisi zinaendeshwa dhidi ya wale wote waliohusika na ukiukwaji huo.

Kituo hicho, katika taarifa iliyochapishwa kupitia tovuti yake katika Siku ya Kimataifa ya Wahanga wa “Kutoweshwa kwa Lazima”, kimesema: “Kutoweshwa kwa lazima” si tu kumweka mtu kizuizini kinyume cha sheria, bali ni ukiukwaji mkubwa unaomweka mwathirika nje ya ulinzi wa sheria na kuinyima familia yake fursa ya kujua hatima yake, huku ikiweka mazingira yanayoweza kusababisha mateso, kutendewa vibaya na hata kifo bila uangalizi madhubuti.

Kituo hicho kimeeleza: Kesi ya shahidi “Sayyid Muhammad al-Mousawi” inaonyesha kwa uchungu hatari ya vitendo hivi. Al-Mousawi alikamatwa tarehe 19 Machi 2026 (29 Esfand 1404) katika kituo cha ukaguzi katika eneo la Muharraq, lakini familia yake haikujulishwa hatima yake kwa muda wa siku tisa; kisha iliitwa katika Hospitali ya Vikosi vya Ulinzi vya Bahrain na kupewa taarifa kwamba amefariki dunia, huku mwili wake ukiwa na majeraha makubwa yaliyolingana na kupigwa mara kwa mara akiwa kizuizini. Kitengo Maalumu cha Uchunguzi kilikiri kwamba kifo chake kilitokana na kupigwa alipokuwa kizuizini.

Kituo cha Haki za Binadamu Bahrain kimesisitiza: Kesi za “kutoweshwa kwa lazima” na mateso haziwezi kuchukuliwa kuwa matukio ya kibinafsi au ya pembeni, bali ni lazima hatua za msingi na za kimuundo za mageuzi zichukuliwe kwa uwajibikaji wa kweli na wenye ufanisi, ili kuzuia ukiukwaji huu kujirudia.

Kituo hicho pia kimeeleza: Mamlaka za Bahrain zinapaswa kusitisha vitendo vyote vya “kutoweshwa kwa lazima”, kuweka wazi mara moja hatima na mahali walipo watu wote waliotoweshwa kwa lazima, na kufanya uchunguzi huru na usio na upendeleo kuhusu visa vyote vya “kutoweshwa kwa lazima”, mateso, kutendewa vibaya na vifo vinavyotokea wakati watu wakiwa kizuizini. Aidha, zinapaswa kuhakikisha uwajibikaji na mifumo madhubuti ya kutoa fidia, ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mbele ya sheria wahusika wa ukiukwaji huo.

Kituo cha Haki za Binadamu Bahrain kimetoa wito wa kuachiliwa raia wote waliowekwa kizuizini kwa sababu tu ya kutumia haki zao za msingi, kukomeshwa kuwekwa kizuizini kwa njia zisizo za haki na kwa makundi, pamoja na aina yoyote ya adhabu ya pamoja. Pia kimetaka waangalizi wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa na waangalizi wengine huru wa kimataifa wapewe fursa isiyo na vikwazo ya kuingia nchini Bahrain, wakiwemo waangalizi wanaohusika na masuala ya mateso na “kutoweshwa kwa lazima”, na kuhakikisha sheria za kitaifa zinatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya haki za binadamu.

Kituo hicho kimeitaka jumuiya ya kimataifa kuongeza kwa haraka zaidi shinikizo dhidi ya mamlaka za Bahrain ili kukomesha “kutoweshwa kwa lazima”, mateso na ukandamizaji wa kimfumo, kushughulikia suala la watu waliopotea na wafungwa, na kuhakikisha kwamba kuhifadhi haki za binadamu kunapewa nafasi ya kwanza katika uhusiano wa kisiasa, kidiplomasia na kiusalama na Bahrain; kwa sababu haiwezekani Bahrain kuzungumzia mageuzi ya kweli wakati vyombo vya ukandamizaji na kukwepa uwajibikaji bado vinaendelea kuwepo.

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha